TAJIRI IBRAHIM SHAYO KASEMA: “TUTAONGEZA MAGARI YA KUZOA KUUWEKA MJI WA MOSHI SAFI"

MOSHI-KILIMANJARO

MGOMBEA wa kiti cha Ubunge kupitia Chama Cha mapinduzi(CCM),mfanyabiashara tajiri ,Ibrahim Shayo maarufu kwa jina la Ibra Line,amesema endapo atachaguliwa kuwa mbunge wa jimbo la moshi mjini,atashirikiana na madiwani watakaounda Baraza la madiwani Manispaa ya Moshi kuhakikisha yanannunuliwa magari zaidi  kwa ajili ya kuzoa taka.

Shayo mmoja wa wafanyabiashara maarufu katika sekta ya mafuta na usafrishaji ,ametoa ahadi hiyo katika mkutano wa kampeni uliofanyika kata ya Mfumuni eneo ya NHC kuelekea uchanguzi Mkuu wa Rais,wabuge na madiwani utakaofanyika Oktoba 29 mwaka huu.

Alisema mji wa moshi ambao unasifika kwa usafi kwa sasa unakabiliwa na mrundikano wa taka unaosababishwa na uhaba wa magari ya kuzoa taka hali inayosababisha baadhi ya maeneo kuwa na mrundikano wa taka.

“Ndugu zangu wananchi niseme wazi kuwa mji wetu kwa sasa unachangamoto ya magari ya kuzoa taka,sasa mkinichagua kuwa mbunge wenu nakwenda kushirikiana na madiwani wenzangu ili tuongeze magari ya kuzoa taka ili kuuweka mji wetu katika hali ya usafi”,alisema.

Mgombea huyo kwa kiti cha ubunge pia alizungumzia msongamano wa magari kwenye barabara ya Double Road  hasa eneo la Mbuyuni ambayo imekuwa kero hasa nyakati za jioni na kuahidi kuweka mkakati wa kuweka Taa za kuongoza magari.

Alizungumzia pia suala la miundombinu ya barabara na kuahidi kushughulikia baadhi ya maeneo yenye changamoto hiyo na kuongeza kuwa atakwenda bungeni kujenga hoja ili serikali iongeze fedha kwenye miundombinu ya barabara katika mji wa moshi.

“Mheshimiwa Rais wetu amefanya mambo mengi mazuri katika mji wetu wa Moshi,ametuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospital yetu ya wilaya inayojengwa kata ya Ng’ambo,ametuletea fedha zikakarabati shule zetu kongwe za sekondari,leo ukienda Mawenzi Sekondari madhari ya shule hiyo ni kama makazi ya mtu binafsi”,alisema.

Aliwataka wanamoshi kumpa kura nyingi Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ili nae apate nguvu ya kwenda kumlilia shida za wanamoshi pale atakapochaguliwa kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi huo wa Oktoba 29 mwaka huu

Mkutano huo pia ulitumika kumnadi mgombea wa kiti cha Udiwani kata ya Mfumuni Stuart Nathaniel Nkini ambaye pia amekuwa Naibu Meya wa manispaa ya Moshi kwa miaka minne na kwa sasa anasubiria kupigiwa kura za ndiyo au hapana baada ya kutopata mpinzani kwenye kata yake.

Kwa upande wake kada mpya wa CCM na ambaye alikuwa mbunge wa viti maalumu(Chadema)katika Bunge lililopita,Felista Njau amemwagia sifa kem kem Ibrahim Shayo kwa mema ambayo amekuwa akiyafanya mara kwa mara akiwa si mbunge.

“Wema unajibiwa kwa wema,tuingieni mitaani tukatafute kura kwa ajili ya Ibra Line,ametufanyia mema hata hajawa mbunge,je akiwa mbunge atatufanyia mema mangapi”,alisema mwanamama huyo ambaye alikuwa mmoja wa watia nia ndani ya CCM jimbo la Moshi Vijijini na kushika nafasi ya tatu.

Mkutano huo wa kampeni pia ulihudhuliwa na mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi(CCM)Moshi mjini,Faraj Kibaya Swai,Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Kilimanjaro,Elizabert Maro Minde,makada mbali mbali na baadhi ya wagombea wa nafasi za udiwani na mgombea huyo anaendelea na kampeni zake kwenye kata za Msaranga,Mawenzi na kwingineko.





Post a Comment

0 Comments