MABAKI YA MWILI WA MTANZANIA JOSHUA MOLLEL ALIYEUAWA NA KUNDI LA HAMAS YAWASILI NCHINI

 

MABAKI ya mwili  wa Mtanzania Joshua Mollel, aliyeuawa na kundi la Hamas katika ukanda wa Gaza miaka miwili iliyopita, yamewasili loe nchini na kupokelewa na ndugu jamaa na marafiki katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa KIlimanjaro (KIA) ukitokea Tel Aviv, Israel.

Kuwasili kwa mabaki hayo ya mwili wa Joshua inafuatia makubaliano ya kumaliza vita katika ukanda wa Gaza na kuruhusu  makabidhiano ya mateka na miili ya waliouawa kwa pande zote kati ya  nchi ya Israel na Kundi la Hamas kutoka Palestina.

Tayari Israel imepokea miili ya mateka 19 Waisraeli waliorejeshwa na Hamas, pamoja na miili ya mateka watatu raia wa kigeni,raia mmoja wa Thailand, mmoja wa Nepal na Mtanzania mmoja.

Kwa upande mwingine Israel  imekabidhi jumla ya miili 285 ya Wapalestina ikiwa ni sehemu ya makubaliano hayo yaliyopelekea kutamatika kwa vita hivyo ambavyo vimagharimu maisha ya watu na mali zao huku maelfu wakiyakimbia makazi yao.

Ibada maalumu ya kuaga mabaki ya mwili wa Joshua  ilifanywa na Ubalozi wa Tanzania nchini Israel siku ya jana Jumanne, Novemba 18 kabla ya safari ya kurejeshwa nchini .



Mollel alikuwa akifanya mafunzo ya kilimo katika eneo la Kusini mwa Israel, kabla ya mashambulizi ya ghafla ya Hamas ya Oktoba 7,2023 nchini Israel yaliyoua watu 1,205 na wengine zaidi ya 200 kuchukuliwa mateka  

Mabaki ya mwili huo yamepokelewa na Ujumbe wa Serikali ya Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania ukiongozwa na  Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa na Balozi Silima Haji Kombo. 

 Mabaki ya Kijana Joshua Mollel yanatarajiwa kuzikwa   kesho  Novemba 20,  2025 mtaa wa Njiro yaliyopo kata ya Orkesumet Wilaya ya Simanjiro,  Mkoani Manyara.

 














Post a Comment

0 Comments