Tanapa yazindua Bodi ya Uendeshaji ya Tanapa Investiment Limited na kupiga hatua kubwa Katika Mageuzi ya Uwekezaji

 Makala hii imeandaliwa na Bahati Nyakiraria na Charles Ndagulla 


SHIRIKA la Hifadhi za Taifa Tanzania(Tanapa)limezindua  Bodi ya Wakurugenzi ya Uendeshaji wa Kampuni Tanzu ya Uwekezaji ya Tanapa  Investment Limited – TIL) na kufungua ukurasa mpya katika historia ya usimamizi wa rasilimali, uwekezaji na uendelevu ndani ya TANAPA.

Tukio hilo lililoongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa TANAPA, Mkuu wa Majeshi Mstaafu Jenerali George Marwa Waitara hivi karibuni, limeonesha dhamira ya dhati ya shirika hilo kuhakikisha usimamizi makini wa miradi yake ya kibiashara sambamba na kuongeza mchango wa uhifadhi katika uchumi wa taifa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Jenerali Waitara aliipongeza Bodi hiyo  kwa kuaminiwa na kukabidhiwa jukumu muhimu la kusimamia TIL, kampuni iliyoanzishwa kwa lengo la kuongeza ufanisi, ubunifu, na tija katika uwekezaji wa TANAPA. 

Waitara  alisisitiza kuwa uteuzi wa wajumbe hao ni matokeo ya kuamini uwezo wao wa kitaaluma na uzoefu wao katika masuala ya uongozi, uchumi, uwekezaji, na uhifadhi.

Jenerali Waitara alitoa wito kwa bodi hiyo kuimarisha misingi ya uwajibikaji, weledi na uwazi katika kutekeleza majukumu yake na kwamba  TIL inahitaji kuongozwa kwa mtazamo mpana utakaowezesha kampuni kujiimarisha katika ushindani wa kibiashara, hususan katika mazingira ya sasa ambapo miradi mingi ya sekta ya umma inasisitiza kutumia utaalamu wa ndani ili kupunguza gharama na kuongeza ufanisi.

Katika hotuba yake, alieleza kuwa bodi inatarajiwa kuanzisha na kusimamia miradi ya kimkakati itakayochochea ukuaji wa mapato ya TANAPA bila kutegemea vyanzo vya jadi pekee.

Hii inajumuisha miradi ya miundombinu ya utalii, majengo, uwekezaji wa kiteknolojia, na huduma shirikishi zinazolenga kuboresha uzoefu wa watalii katika hifadhi za taifa.

 Serikali, kupitia Bodi ya Wadhamini na menejimenti ya TANAPA, imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuibua vyanzo vipya vya mapato ili kuimarisha uhifadhi na kutunza maliasili za taifa.

Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini ya  shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania(Tanapa),Mkuu wa Majeshi Mstaafu ,Jenerali  George Mwita Waitara

 Jenerali Waitara amesema wajumbe wa bodi wanategemewa kuwa chachu ya kuleta ubunifu na mtazamo wa kimkakati katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

 Dira hiyo inasisitiza uhifadhi endelevu, matumizi ya teknolojia, na uwekezaji katika miradi yenye manufaa kwa jamii.kwa mantiki hiyo, TIL inapaswa kuwa mfano wa taasisi za serikali zinazochanganya biashara na uhifadhi kwa ufanisi unaoleta matokeo halisi.

Kwa upande wake, Kamishna wa Uhifadhi wa TANAPA, CPA Mussa Nasoro Kuji, alisisitiza kuwa uzinduzi wa bodi hiyo unaendana moja kwa moja na juhudi za serikali ya awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Alibainisha kuwa serikali imeweka mazingira bora ya uwekezaji na mageuzi ya kiuchumi, hasa katika sekta ya utalii na uhifadhi ambazo zinazidi kuwa nguzo muhimu za mapato ya taifa.

Aidha, alieleza kuwa TANAPA imejipanga kikamilifu kuhakikisha kuwa mageuzi yanayotekelezwa na serikali yanaenda sambamba na ukuaji wa sekta ya uhifadhi kwa kuanzisha miradi inayochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

CPA Kuji aliongeza kuwa TIL inayo nafasi muhimu katika kuhakikisha kwamba miradi ya TANAPA inatekelezwa kwa ufanisi unaotakiwa, ikiwa ni pamoja na kuongeza thamani ya maeneo ya hifadhi, kuboresha miundombinu na huduma zinazowavutia watalii wa ndani na nje.

Aidha, alisisitiza kuwa uwekezaji utakaofanywa kupitia TIL utapaswa kuwa na uhusiano wa moja kwa moja na malengo ya uhifadhi na maendeleo ya jamii zinazozunguka hifadhi.

Naye Mtendaji Mkuu wa TIL, Mhandisi Dkt. Richard Matolo, aliweka wazi dira ya kampuni hiyo huku akitoa msisitizo juu ya matumizi ya utaalamu wa hali ya juu na teknolojia katika kuendesha miradi ya ukandarasi.

Dkt. Matolo alieleza kuwa TIL imejiandaa kikamilifu kuleta mapinduzi katika sekta ya ukandarasi kwa kuhakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati, kwa ubora wa juu, na kwa gharama zinazowiana na thamani ya kazi.

Kwa mtazamo wake, matumizi ya teknolojia za kisasa sio tu yataboresha ufanisi wa kazi, bali pia yatapunguza utegemezi wa wakandarasi kutoka nje ya taasisi.

 Hii itasaidia TANAPA kuwa na udhibiti mkubwa wa miradi, kupunguza gharama za uendeshaji, na kuimarisha uwezo wa ndani wa kitaalamu.

Mbali na hilo, Dkt. Matolo alisisitiza kuwa TIL itakuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa miradi inaendana na viwango vya kimataifa vya ukandarasi na ujenzi, hatua itakayoongeza hadhi ya kampuni katika soko la ndani na nje.

Kwa ujumla, uzinduzi huu umeleta matumaini makubwa kwa wadau wa uhifadhi, utalii na uwekezaji nchini.ni hatua muhimu katika kuelekea kujenga taasisi imara ya kibiashara ndani ya TANAPA ambayo si tu itahakikisha mapato endelevu, bali pia itachangia kwa kiasi kikubwa kwenye uhifadhi wa rasilimali za taifa na kuboresha ustawi wa jamii.

TIL, ikiwa na bodi mpya yenye uzoefu na maono mapana, inatarajiwa kutoa mchango mkubwa katika kuleta mageuzi chanya katika uwekezaji na utekelezaji wa miradi ya kimkakati. Huu ni mwanzo mzuri unaoashiria mustakabali wenye matumaini makubwa kwa sekta ya uhifadhi na tasnia ya utalii kwa ujumla.

 



Post a Comment

0 Comments